Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mhe. Josephine Manase, tarehe 09 Februari 2026 amezindua rasmi zoezi la ugawaji wa Kadi za Bima ya Afya kwa Wote kwa kaya maskini katika hafla iliyofanyika Kata ya Bondeni, wilayani Kyela.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mhe. Manase amesema kuwa awamu ya kwanza ya zoezi hilo inalenga kuandikisha kaya maskini, ambapo walengwa watasajiliwa na kupatiwa vitambulisho vya bima ya afya vitakavyowawezesha kupata huduma za matibabu kwa kipindi cha mwaka mzima bila gharama yoyote. Amesisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imechukua jukumu la kugharamia bima hizo ili kuhakikisha wananchi wenye uhitaji wanapata huduma za afya bila vikwazo vya kifedha.

Ameeleza kuwa katika awamu ya kwanza, jumla ya walengwa 6,731 sawa na Kaya 1881 watafikiwa katika kata zote za Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, kwa lengo la kuwaandikisha na kuwawezesha kunufaika na huduma za bima ya afya. Hatua hiyo ni utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuboresha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi wote.
Aidha, Mhe. Manase amewataka wananchi wa Kata ya Bondeni kuwa mabalozi wa kuhamasisha wenzao kujitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi hilo, akisisitiza kuwa fursa hiyo ni muhimu kwa ustawi wa afya za familia na jamii kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, Adv. Florah A. Luhala, amewataka wananchi waliopata kadi hizo kuzitunza na kuzitumia kwa matumizi sahihi, akionya dhidi ya kuzitoa kwa watu wengine kwani kufanya hivyo ni kinyume cha taratibu za matumizi ya bima ya afya.

Kwa niaba ya Wananchi wa Kata ya Bondeni, Bi. Victoria Mwaitenda, amemshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwaletea wananchi mpango huo muhimu, akisema umewaletea matumaini mapya ya kupata matibabu bila hofu ya gharama. Amesema hatua hiyo itaondoa adha kubwa iliyokuwa ikiikumba familia nyingi zenye kipato cha chini.

Ikumbukwe kuwa zoezi la uandikishaji wa Bima ya Afya kwa Wote ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa Serikali unaolenga kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma za afya kwa gharama nafuu kupitia mfumo wa bima ya afya, hatua inayochochea ustawi wa jamii na maendeleo ya taifa kwa ujumla.
Bomani Street
Sanduku la Posta: P. O box 320 Kyela
Simu ya Mezani: 025-2540035/7
Simu ya Mkononi: 0713655466
Barua pepe: ded@kyeladc.go.tz
Haki miliki @2017 Halmashauri ya wilaya ya Kyela. Haki zote zimehifadhiwa