Halmashauri ya Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya imeibuka mshindi wa tatu kitaifa katika kipengele cha matumizi ya TEHAMA kwa kushirikisha wananchi, katika Kikao Kazi cha Sita cha Serikali Mtandao (eGA). Kikao hicho kilifanyika kuanzia tarehe 17 hadi 19 Februari 2026 katika ukumbi wa kimataifa wa Arusha International Conference Centre jijini Arusha, ambapo mgeni rasmi wa ufunguzi alikuwa Moses Kusiluka, Katibu Mkuu Kiongozi.

Tuzo hiyo ilitolewa na Mhe. Ridhiwani Kikwete, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga kikao hicho tarehe 19 Februari 2026. Kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, tuzo hiyo ilipokelewa na Afisa TEHAMA wilaya ya Kyela, Ndg. Bwigane Amlike.

Kikao kazi hicho kilikuwa na kauli mbiu isemayo: “Kubadili na kuboresha uendeshaji wa shughuli za Serikali kwa kuimarisha utoaji wa huduma kwa umma kupitia mifumo jumuishi na salama ya Serikali kidijitali.” Mada hiyo imelenga kuhamasisha taasisi za umma kuimarisha matumizi ya teknolojia za kidijitali ili kuongeza ufanisi, usalama wa mifumo na ushirikishwaji wa wananchi katika huduma za kijamii.

Ushindi huo unaonesha juhudi na dhamira ya Halmashauri ya Wilaya ya Kyela katika kutumia mifumo ya TEHAMA kuboresha mawasiliano, uwazi na ushirikishwaji wa wananchi katika huduma mbalimbali za kijamii. Aidha, ni kielelezo cha namna halmashauri ya Kyela inavyoendana na mabadiliko ya teknolojia na kuunga mkono kikamilifu utekelezaji wa Serikali Mtandao nchini.

Bomani Street
Sanduku la Posta: P. O box 320 Kyela
Simu ya Mezani: 025-2540035/7
Simu ya Mkononi: 0713655466
Barua pepe: ded@kyeladc.go.tz
Haki miliki @2017 Halmashauri ya wilaya ya Kyela. Haki zote zimehifadhiwa