Haya yamezungumzwa na Meneja wa Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) kanda ya nyanda za juu kusini Bi. Anitha Mshigati alipokuwa akitoa elimu juu ya kuzitambua dawa bora kwa matumizi ya binadamu pamoja na vifaa tiba, kwa wajasiriamali na wanafunzi hapa wilayani Kyela.
Elimu hiyo imetolewa katika shule ya sekondari Nkuyu na shule ya sekondari Kajunjumele ikijumuisha wanafunzi, walimu pamoja na wajasiriamali kutoka vikundi mbalimbali vilivyopo hapa wilayani Kyela, tarehe 07/10/2022.
Akitoa elimu kwa walimu, wanafunzi na wajasiriamali hao Meneja wa TMDA Bi. Anitha amesema Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba kwa kupitia wataalam wake, hupita na kufanya ukaguzi katika maeneo mbalimbali yakiwemo maeneo ya hospitali, vituo vya afya, zahanati pamoja na maduka ya madawa ili kujiridhisha na utunzaji mzuri wa dawa. Kwani dawa zisipotunzwa vizuri zaweza haribika na kuleta madhara kwa binadamu au wanyama.
Amesema zoezi la ukaguzi wa dawa ni sehemu ya majukumu ya TMDA lakini pamoja na hayo TMDA imekuwa ikifanya kaguzi za mara kwa mara katika maeneo yanayotoa huduma za dawa ikiwemo maduka ya dawa za mifugo. Haya yote yanafanywa ili kujihakikishia kuwa dawa zote zilizokaguliwa na kupewa vibali na Mamlaka ya Dawa, zinatunzwa vizuri, pia ndizo dawa kweli zilizopo kwa matumizi halali kwa binadamu na wanyama.
"Lakini pia tunasimamia majaribio ya matumizi ya dawa mbalimbali, ambapo tunahakikisha taratibu zote za majaribio ya dawa za binadamu yanafuata sheria na taratibu zilizowekwa bila usumbufu wowote kwa wananchi" alisema Bi Anitha Mshigati.
Aidha Amesema Mamlaka ya dawa na vifaa Tiba TMDA hufuatilia dawa zote zinazotumiwa na wananchi ili kujua kama zinamadahara kwa baadhi ya wananchi, na endapo litabainika hilo, basi dawa hilyo huondolewa katika soko ili kumlinda mwananchi.
Richard Mbwile Mwanafunzi wa shule ya sekondari Nkuyu alipata fulsa ya kuuliza swali ikiwa kama atapata wasiwasi na dawa ambazo amezinunua katika duka la dawa atafanyaje, swali hilo lilijibiwa vizuri na Bi. Grace Kapande Mkaguzi wa Dawa TMDA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini kwa kumshauri ndugu Richard kufika katika kituo chochote cha afya kilichopo karibu nae au kupiga namba 0800110084 ili kipata maelezo sahihi ya juu dawa hizo.
Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) ni taasisi ya serikali iliyochini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, yenye jukumu la kulinda afya ya jamii kwa kuhakikisha bidhaa za dawa, vifaa tiba na vitendanishi ni salama, bora na fanisi kwa matumizi ya binadamu na mifugo.
Pia TMDA imekasimishwa majukumu ya kudhibiti bidhaa za tumbaku ili kupunguza athari zake kwa binadamu.
Mwisho.
Bomani Street
Sanduku la Posta: P. O box 320 Kyela
Simu ya Mezani: 025-2540035/7
Simu ya Mkononi: 0713655466
Barua pepe: ded@kyeladc.go.tz
Haki miliki @2017 Halmashauri ya wilaya ya Kyela. Haki zote zimehifadhiwa