Halmashauri ya wilaya Kyela, imefanikiwa kuvuka lengo la kukusanya mapato kwa asilimia 103, ambapo ilitakiwa kukusanya mapato ya sh.bilioni 3.8, na kufanikiwa kukusanya sh.bilioni 3.9, huku bajeti ya mwaka 2022/2023 ikiweka lengo la kukusanya sh.bilioni 4.6.
Imeelezwa, Halmashauri imekuwa ikivuka lengo la makusanyo, ambapo mwaka 2022 bajeti ilikuwa sh.bilioni 3.6, mwaka 2021/2022 ikafikia sh.bilioni 3.9, na bajeti ya mwaka 2022/2023 imefikia sh.bilioni 4.6.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya Kyela, Katule G. Kingamkono, aliyasema hayo katika mkutano wa Baraza la madiwani, kupitisha hesabu za Halmashauri, kwa mwaka 2021/2022, uliofanyika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri uliopo Kyela Mjini tarehe 28/09/2022.
“Tunampongeza Rais Samia Suluhu Hassan, kwani katika bajeti yetu hii ya mwaka 2021/2022 tumepokea zaidi ya sh.bilioni 35.6, ambazo zinajumuisha mishahara ya watumishi na shughuli nyingine zote za maendeleo” alisema Kingamkono.
Alisema katika bajeti iliyopita, ilipanga lengo la kukusanya sh.bilioni 3.8 lakini imevuka lengo kwa asilimia 103, ambapo tumefanikiwa kukusanya sh.bilioni 3.9, na katika bajeti ya mwaka 2022/2023, baada ya kuona tumeendelea kufanya vizuri, Halmashauri imeamua kubuni vyanzo vingine vya mapato ili kuongeza mapato katika halmashauri yetu.
“Hivyo bajeti imekwenda hadi kufikia sh.bilioni 4.6, ambayo tunayo uhakika wa kuikusanya sababu tumejipima, tangu tumeanza mwaka 2020 tumekuwa tunapanda kila mwaka hivyo hata hii tutaweza” alisema Kingamkono.
Aliongeza mwaka 2020 bajeti ilikuwa sh.bilioni 3.6, mwaka uliofuata ikafika sh.bilioni 3.9 na sasa bajeti ya mwaka 2022/2023 imefikia sh.bilioni 4.6, Hii inatokana na umoja na mshikamano na katika baraza la madiwani wametulia.
Kingamkono alisema pia timu ya wataalam wa Halmshauri, imejipanga vizuri, ofisi ya mkuu wa wilaya inatoa ushirikiano, ofisi ya mbunge pamoja na mbunge mwenyewe, na wanaendelea kusimamia vyema ili kuhakikisha Ilani ya Uchaguzi ya CCM inatekelezwa.
Mwenyekiti huyo alisema lengo ni kuhakikisha miradi ya maendeleo inakwenda, lakini pia wanaendelea kukopesha vikundi kama vile Ilani ya Uchaguzi ya CCM inavyoelekeza.
Alisema hakuna maendeleo yanayopatikana bila umoja na mshikamano, kwa hiyo umoja wao ndiyo ambao umetoa dira lakini pili wamezingatia sana kusimamia uadirifu na nidhamu, kuhakikisha fedha yoyote inayokusanywa, inaingizwa katika akaunti kama utaratibu wa serikali za mitaa unavyoeleza.
“Pamoja na mimi kuwa Mwenyekiti wa halmashauri , lakini waheshimiwa madiwani tunacheza timu mmoja” alisema Kingamkono.
Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri Kyela, Ndugu Ezekiel H. Magehema, alisema Halmashauri imetoa mikopo kwa vikundi mbalimbali, ambapo wanawake na vijana walipata sh.milioni 107 kila kundi, huku watu wenye ulemavu wakipata sh.milioni 50.
Magehame alisema fedha hiyo ilitokana na asilimia kumi ya mapato wanayokusanya ukiachilia mbali marejesho ya fedha kutoka katika mikopo hiyo.
Aliongeza kwa kusema, katika mwaka huu wa fedha tumejipanga, Na mfumo uliopo umesaidia sana katika ufungaji wa hesabu za serikali, Pia mfumo huu unatusaidia katika matumizi ya kawaida ya fedha ambayo Halmashauri inakusanya mapato yake kwa njia ya mfumo.
“Tunazidi kuimarisha vitendea kazi ili tuwe na vifaa vya kutosha vya kukusanyia mapato, tuhakikishe vijana wetu wanaokusanya mapato, kwa maana ya mawakala na maofisa watendaji wa serikali za vijiji na kata, wanakusanya fedha zote na zinapelekwa benki” alisema Magehema.
Diwani wa kata ya Njisi, Omary Mwijuma, aliipongeza serikali ya CCM inayoongozwa na Rais Samia Sluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi wilayani Kyela, na kwamba fedha ya elimu bila malipo imewasaidia wananchi wa chini, na kuwawezesha watoto wao kupata elimu.
Bomani Street
Sanduku la Posta: P. O box 320 Kyela
Simu ya Mezani: 025-2540035/7
Simu ya Mkononi: 0713655466
Barua pepe: ded@kyeladc.go.tz
Haki miliki @2017 Halmashauri ya wilaya ya Kyela. Haki zote zimehifadhiwa